Wafugaji waiangukia serikali kudhibiti ubora wa vifaranga na vyakula vya kuku wa nyama

 
Bertha Mollel - Arusha. 

. Kutokana na vifo vingi vya vifaranga vinavyowatokea kwenye mabanda na vyakula kushindwa kukuza kuku kwa mda unaotakiwa wafugaji nchini wameiomba serikali kudhibiti makampuni yanayotoa vifaranga na vyakula vya kuku wa nyama visivyo na ubora kwani vinawadidimiza kiuchumi.
 
Hayo yamesemwa na wafugaji wa kuku wa nyama (Broiler) kwenye mkutano wa siku moja uliowakutanisha wafanya biashara wa kuku na wafugaji  kutoka mikoa ya Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Tanga na Dodoma iliyoitishwa na Kampuni ya bidhaa asilia za kuku cha 'Trouw nutrition'
 
Mmoja wa wafugaji Beatrice Mlay kutoka Moshi anaefuga kuku 500 alisema kuwa ufugaji wa kuku umekuwa na changamoto nyingi zinazokatisha tamaa ya kuendesha shughuli hiyo huku baadhi ya makampuni wakitoa bidhaa zisizo na ubora hali inayowadidimiza kiuchumi.
 
"Miaka ya nyuma ufugaji ulikuwa unalipa sana kiasi cha kuwa shughuli ya kipaumbele kwa vijana wasio na ajira au wazee wanaostaafu lakini kwa sasa imekuwa inatunyonya hata mitaji yetu kutokana na baadhi ya makampuni kutokuwa waaminifu na bidhaa wanazotuuzia kwa kupunja baadhi ya virutubisho kwenye vyakula ili kujipatia faida" alisema na kuongeza...
 
"Tunaomba serikali ifanye msako wa viwanda vya vyakula bubu na wale wanazotengeneza vyakula vizivyo na ubora wafungiwe,  pia mashamba ya kuzalisha vifaranga wakaguliwe maana siku hizi vifaranga vingi feki havina ubora vinakufa vikifika bandani na wengine kudumaa bila kukua kwa muda tarajiwa"
 
Alisema katika banda lake analoingiza kuku 500 kuanzia siku ya kwanza hadi siku 35 anayopaswa kuuza, hupoteza zaidi ya kuku 50 hadi 100 inayotokana na vifaranga dhaifu, lakini pia ubora wa vyakula mdogo tena vingine vikiwa na sumu kuvu ambayo huharibu mfumo mzima wa kupitisha chakula kwa kuku.
 
Nae Charles Shauri anaefuga kuku 1000 alisema kuwa changamoto inayowakabili ni bei ndogo ya kuku ya shilingi 6500 kwa mmoja huku kukiwa na bei kubwa ya vyakula vya kuku wa nyama iliyokuwa inauzwa shilingi 60,000 hadi 65,000 kwa kiroba cha kilo 50 mwaka 2020 sasa ni 85,000 hadi 90,000 hali ambayo imepandisha pia bei ya vifaranga kutoka shilingi 1500 hadi 2000 kwa kimoja

 
" Tatizo ni uhaba wa nafaka na protini iliyotokana na kukumbwa na mabadiliko ya tabia ya nchi hasa ukame kiasi cha wafanyabiashara wa chakula kutupandishia bei kulingana na wanavyopata lakini kupunja baadhi ya protini na virutubisho kwenye kuchanganya vyakula hii inawafanya kuku kuishi bandani  kwa zaidi ya siku tano hadi 10 za ziada kutoka Ile 30 hadi 35 anayopaswa kuuzwa"
 
"Mbaya zaidi unakuta chakula hakuna ubora hivyo unapompa kuku unaweza kumsababishia kudumaa au kupata magonjwa mbali mbali yanayopelekea vifo kwa kukosa virutubisho muhim au magonjwa yatokanayo na sumu kuvu endapo malighafi za kutengeneza chakula hayakuhifadhiwa vyema"
 
 Alisema kuwa kutokana na hayo wafugaji wamekuwa watumwa wa kutumia madawa mbali mbali na kemikali za hatari kukuzia kuku bila kujali  afya za walaji ili tu kunusuru biashara zao
 
 
Nae meneja wa kampuni ya bidhaa za kuku kutoka trouw Nutrition,  Joseph Joachim Alisema kuwa wako jijini Arusha kuwapa mafunzo zaidi wafugaji jinsi ya kutumia bidhaa za asili kutoka vya mimea na matunda kukuzia kuku bila madawa yenye kemikali zinazoathiri zaidi walaji wao ambao ni binadamu.
 
Alisema kuwa changamoto kubwa katika ufugaji ni magonjwa mbali mbali yanayowapata kuku inayotoka na asili ya kifaranga alipototolewa, hali ya hewa, maji na chakula hasa visivyo na virutubisho vya kutosha au vilivyopatwa na ugonjwa sumu kuvu.
 
"Haya yote yanawalazimu wafugaji kutumia madawa mengi hata yaliyo hatari kwa walaji kwa kusababisha magojwa ya kansa lakini watatumia kuokoa kuku wao, kutokana na hilo tumekuja kuwapa  suluhu la bidhaa kadhaa za kuwasaidia kutibu kifaranga akiwa mdogo, maji yao ya kunywa lakini pia virutubisho mbali mbali vya chakula Ili kuokoa kuku kudumaa na hizi hazina madhara wala kemikali" 
 
Alisema kuwa sekta ya ufugaji wa kuku unakua zaidi nchini kutoka kuku milioni 44 kwa miaka mitano iliyopita hadi milioni 92 pamoja na changamoto nyingi zinazokatisha tamaa wanazokabiliana nazo hasa chakula kuwa ghali na vifaranga huku bei ya kuku ikibakia ndogo hivyo kuiomba serikali kutoa bei elekezi ya vyakula vya kuku na kuku wenyewe sokoni.
 

Post a Comment (0)
Previous Post Next Post
Alert: Content is protected !!